HISTORIA YA MAREHEM SHEKH MUHAMMAD MUSSA MZIMBIRI (1959 - 2020)

Àalim Rabbani, Mlezi wa Maadili, Mwanga na Fakhari ya Milima ya Usambara 1.UTANGULIZI; Takriban Miaka 65 iliyopita Katika milima yenye hewa nzuri na mandhari tulivu ya kuvutia ya Usambara, kijiji cha Tema kitongoji cha kwekele kilishuhudia kuzaliwa kwa nuru ya elimu na hekima ambayo ni Sheikh Muhammad bin Mussa Mzimbiri, mmoja wa wanazuoni maarufu wa Milima ya Usambara, Wilaya ya Lushoto Tanga Tanzania aliyetoa maisha yake yote kwa ajili ya Kumtumikia Allah(S.Wt) akiutumikia Uislamu, kusambaza Elimu na kulea jamii kwa maneno na vitendo. Alikuwa alama ya taq'wa, maarifa, na unyenyekevu wa hali ya juu. 2.JINA LAKE NA NASABA YAKE; Jina lake kamili ni: Sheikh Muhammad bin Mussa bin Mzimbiri bin Mpemba bin Kimweri bin Mbega Al-Kindiyy At-Tamtiyy Nasabu yake alitokana na ukoo mashuhuri wa viongozi wa kimila na kidini katika milima ya Usambara. Baba yake Sheikh Mussa Mzimbiri Mpemba, alikuwa miongoni mwa machifu maarufu wa eneo hilo, aliyejulikana kwa uadilifu na uchamungu wake na kupenda ilmu na kuitukuza, Na Ammi yake(baba mdogo) Shekh Sufian Mzimbiri alikuwa ni Shekh Wa Wilaya Ya Lushoto katika zama zake. 3.KUZALIWA NA MALEZI YAKE Shekh Muhammad Mzimbiri Alizaliwa siku ya Jumatano, tarehe 07 Oktoba 1959, katika kijiji cha Tema, kitongoji cha Kwekele, Kata ya Sunga, Wilaya ya Lushoto, Mkoa wa Tanga Nchi ya Tanzania. Mama yake mpendwa aliitwa Zainabu bint Muhammad, maarufu kama Bibi Suse, ambaye ni miongoni mwa wake wanne wa mzee Mussa Mzimbiri Mpemba,..Sheikh Muhammad alikuwa ni mtoto wa tatu kati ya watoto 9 wa mama yake. Alikulia katika mazingira ya kijijini yaliyojaa maadili ya dini, heshima kwa wakubwa, ukarimu na moyo wa kuhudumia jamii. Shekh Muhammad Mzimbiri Aliacha Wajane wanne,(4) watoto 21(ambapo wakiume wapo 13 na wakike wapo 8) na wajukuu 18. 4.MWANZO WA SAFARI YA KUTAFUTA ELIMU YA DINI NA SECULAR ■Elimu Ya Secular/Dunia Mwaka 1972 Shekh Muhammad Alijiunga na Shule Ya Msingi Mambo (Mambo Primary School) ambayo iko kijiji cha Mambo na kumaliza mwaka 1978, hakuendelea mara alipomaliza Darasa la 7. ■Elimu Ya Dini/Akhera Masomo ya Awali – Kwa Sheikh Rashid Shemndolwa Marhoom Shekh Muhammad Mussa Mzimbiri alianza kujifunza dini kwa Sheikh Rashid Ally Shemndolwa,(aliyekuwa Shekh Wa Kata Ya Sunga) ambaye naye alisoma kwa Sheikh Sufian Mzimbiri(aliyekuwa Shekh Wa Wilaya Ya Lushoto katika Uhai wake) Allah awaraham. Na huko kwa Shekh Rashidi ndiko ambako Shekh Muhammad alipata msingi madhubuti wa elimu ya Dini ya Kiislamu pamoja na malezi bora ya kiroho kutoka kwa Shekh Rashidi kwani aliweza kusoma kwa shekh mpaka akahitimu na akawa ni miongoni mwa walimu na wasomaji wazuri wa Maulid, Khutba za Ijumaa na Tawassul kama Twaibul asmaai n.k Sheikh Muhammad Mzimbiri alimtumikia sana Sheikh Rashid kwa adabu na heshima ya hali ya juu mno na kupata baraka nyingi toka kwa Shekh Rashid Allah Amraham– Akifanya kazi za nyumbani kwa Shekh na mashambani kwa moyo wa utiifu bila kuchoka,. Huduma hizi zilimletea baraka nyingi mno, Radhi na Dua kutoka kwa Sheikh wake. Mama yake Shekh Muhammad (Bibi Suse Allah Amraham) pia alijitolea kwa hali na mali katika kusoma kwa mwanae Alikitoa sadaka za kuku mara kwa mara kumpelekea Sheikh Rashid, kama mchango wa kushukuru maendeleo ya mwanawe. Wazee maarufu na wachamungu wa kijiji cha Tema kitongoji cha kishurui, wakiongozwa na Mzee Ali Athuman Shelufumo na Mzee Hamad Athuman Shelufumo (Allah Awaraham) Walimkataza mama yake Shekh Muhammad Mzimbiri kumtuma kazi za nyumbani wakisema: > “Huyu si mtoto tena, huyu ni Sheikh!” Hivyo alitabiriwa kuwa mwanazuoni tangu yungali kijana mdogo. 5.SAFARI YAKE YA KUSAKA ELIMU YA JUU; Mwaka 1978 – Chuo cha Shadhiliyah Mgombezi Baada ya kupata ruhusa ya Sheikh wake Rashid(Allah Amraham), mwaka 1978, Shekh Muhammad alitoka kwenda kuongeza Elimu na alijiunga na Chuo cha Shadhiliyah Mgombezi, Chini Ya Mudiri wa Chuo hicho Shekh Nurdin bin Hussein akipelekwa na kaka yake Hassan Mussa Mzimbiri, aliyekuwa mwalimu wa masomo ya secular kipindi hicho. Na Huko alifanikiwa kuongeza maarifa yake ya msingi katika fani mbalimbali za elimu ya Dini Ya Kiislamu. Mwaka 1980 – Tanga Mjini, Kwa Sheikh Muhammad Mkanga Shekh Muhammad Mzimbiri alitoka Mgombezi na kuelekea Tanga Mjini kuendelea na safari yake ya kuitafuta ilmu ya Dini Akasoma kwa Sheikh Muhammad Mkanga, aliyekuwa Sheikh wa Mkoa wa Tanga kipindi hicho na huko alikamilisha baadhi ya fani muhimu za elimu ya fiqhi, tafsiri, hadithi, na lugha. Mwaka 1983 – 1990: Madrasat Shamsiyyah (TAMTA) Mnamo mwaka 1983, Shekh alijiunga Rasmi na Madrasa kongwe na maarufu Nchini Tanzania na Duniani kote ambayo ni Shamsiyyah, maarufu kama TAMTA iliyopo Tanga Mjini. Na alipofika hapa ndio akaweka kituo chake cha kudumu na ikawa hii ndiyo taasisi aliyokaa kwa muda mrefu zaidi. Alisoma kwa walimu wengi mashuhuri na wabobezi wa fani ngumungumu wa wakati huo chuoni hapo na wengine wakiwa wangali hai mpaka sasa, na chini ya usimamizi wa Sheikh Muhammad Ayyoub Hamis Al-Kamaadhiy. WALIMU WAKE WAKUU TAMTA 1. Sheikh Yuusuf Subky Ambaye kwa sasa ana miliki Taasisi yake Kubwa ya Kiislam ndani Ya Jiji La Dar-Es-Salaam 2. Sheikh Muhammad Bakari Al-Burhaan– Muasisi wa Shamsil Ma’arifa 3. Sheikh Shareef Muhammad Hashim 4. Sheikh Shareef Sururu Hashimu 5. Sheikh Abdallah Ayoub(maarufu kwa jina la Mushriful Àam) –ambaye ni mdogo wa Sheikh Muhammad Ayoub 6. Wote wakiwa chini ya Mudiri, Àlimul Allama Baba Wa Elimu Tanzania Sheikh Muhammad bin Shekh Ayyoub Hamis Al-Kamaadhiyy– Msimamizi Mkuu KAZI YA UALIMU TAMTA; Shekh Muhammad Mussa Mzimbiri akiwa bado mwanafunzi hapo TAMTA, alichaguliwa kuwa mwalimu wa TAMTA kwa takriban miaka minne, jambo lililoonesha kiwango chake cha juu cha maarifa na heshima aliyopewa. Alifundisha fani kama: ●Nahwu ●Swarf ●Fiqh ●Tajwid na nyingine nyingi Shekh alikuwa mwenye hifdhi na Dhwabt kubwa ya hadithi, akihifadhi zaidi ya hadithi elfu mbili. ☆WANAFUNZI WENZAKE WALIOSOMA PAMOJA MIONGONI MWAO DARSA MOJA NI; 1.Shekh Walid Alhad Omar Kawambwa, ambaye ni Shekh Mkuu Wa Mkoa Wa Dar-Es-Salaam na Imamu mkuu wa Msikiti wa Kichangani 2.Shekh Muhammad Konsel Naibu Chief Kadh Mkuu Tanzania 3.Marehem Shekh Muhammad Idd Abuu Idd Allah Amraham 4.Shekh Muhammad Hamisi Wa Mlalo ambaye ni kadhi wa Wilaya Ya Lushoto Na wengine wengi 6.KUREJEA TEMA NA KUANZISHA MADRASA; Mwaka 1990 – Madrasa ya Shamsiyya Tema Baada ya kuhitimu, aliruhusiwa na Shekh Muhammad Ayyoub kurejea kijijini kwao Tema Kwekele, ambako alianzisha Madrasa ya Shamsiyya, tawi rasmi la TAMTA. Na hii ilikuwa kazi yake kuu ya maisha. Ambapo alianza kufundishia chini ya Mti na baadae Alijenga taasisi hiyo akifundisha kwa moyo, juhudi na hekima ya hali ya juu. Madrasa hii ilizalisha wanafunzi wengi mno wa kike na kiume wazee na vijana ambao wengine ni Walimu Mashekh Na Maimamu waliotawanyika ndani ya Mikoa ya Tanzania 7. WANAFUNZI MAARUFU ALIO WAFUNDISHA NA KUWALEA; 1. Sheikh Jaafari Mussa Mzimbiri – Mdogo wa Shekh, Ambaye Kwa sasa ndiye Mudiri wa Tawi hilo la Madrasa Shamsiyya, Na Shekh Jaafar Ndiye Mwanafunzi Wa Kwanza Na Mkubwa Wa Shekh Muhammad Mzimbiri ambaye alianza kufundishwa Ni Shekh tangu wakiwa Mjini Tanga na kuendelea kufundishwa waliporudi kijijini ambapo alifundishwa fani mbalimbali kama Nahaw, fiqh, Tawheed, sira, taswauf, Hadith, mustwalahul hadith, tafsiri na lugha ya kiarabu, nk. 2. Mwalimu Hassan Mussa Mzimbiri – Ambaye yeye ndiye mwanafunzi wakwanza Wa Shekh Muhammad maratu aliporudi kijijini na pia yeye ni Kaka Mkubwa Wa Shekh Muhammad Mzimbiri, Mwalimu Hassan Pia Alikuwa ni Mwalimu Wa Shule Za Secular ambapo akifundisha Secular na Akifundisha Dini baada ya kuchota Maalumaat kutoka kwa Mdogo wake Shekh Muhammad Mzimbiri. 3. Ustadh Abdallah Muhammad – Mzaliwa Wa Dar-Es-Salaam Na Muasisi wa taasisi kadhaa za Madrasa Jijini Dar es Salaam. 4. Ustadh Qaasim bin Suleiman – Mwalimu Wa Madrasa Korogwe 5. Ustadh Hamza Muhammad – Mwalimu Wa Madrasa Kilimanjaro 6. Ustadh Ally Khalid –Mwalimu Wa Madrasa na Imamu Mkuu Msikiti wa Tema 7. Ustadh Rashid Ally Shemndolwa 8. Ustadh Twaahir Juma Amiri 9. Shekh Almas, Mwalimu wa Madrasa na Imamu Msikiti Mambo Chumbageni 10. Ustadh Issa Msengakamba 11. Ustadh Othman Hassan Mussa Mzimbiri 12. Ustadh Ally bin Yuusuf ambaye yuko Wilaya Ya Handeni akiwa na Madrasa yake huko. 13. Ustadhat Sakina bint Shekh Ally Rashid Shemndolwa 14. Ustadhat Biasha bint Jumaa(huko ndungu kilimanjaro) 15. Ustadhat Khadija bint Hassan (huko ndungu Kilimanjaro) Na wengine wengi waliobarikiwa kupita mikononi mwake waliotapakaa katika mikoa ya Tanzania. KUWAPA ELIMU WATOTO WAKE; Shekh Muhammad alikuwa Baba bora mwenye mapenzi makubwa na huruma kwa watoto wake wote. Alihakikisha anawarithisha watoto wake wote elmu ya Dini akiwasomesha kwa nguvu zake zote, hakutaka mchezo katika swala linalohusu Elimu Pia alijinyima na akahakikisha kwamba japo na kazi yake ya Kufundisha Dini isiyokuwa na mshahara nilazima kuwapa watoto elimu ya Mazingira/Dunia, hakubagua elimu aliamini elimu zote mbili ni Muhimu mno kwa mwanadamu Kwake Elimu ndiyo ilikuwa kipaombele chake, damu yake ilifungamana na ilmu, Alichagua kuwapa watoto wake Dunia na Akhera lakini akihimiza kushika zaidi ilmu ya akhera Kwa jitihada zake za kuwasomesha Watoto wake Dini imefikia hata wale walio ajiriwa Serikalini wamekuwa wakiendelea kusimama Imara katika kuipeleka mbele Dini, Mfano wa watoto wake ambao huko waliko ni waajiriwa Serikalini na wanaishukhulikia Dini ni Ustadh Ally Bin Shekh Muhammad Mussa Mzimbiri Ambaye Ni Mtoto Wa Shekh ambaye ni Mjumbe wa Baraza la Ulamaa kata ya Bondeni Wilaya ya Hai Mkoa wa Kilimanjaro, Ambaye pia ni Afisa Da'awa wa kata ya Bondeni na Imamu Mkuu wa Masjid Minaa. 8.UONGOZI; Kwa elimu yake, tabia na heshima yake, Shekh Muhammad Mzimbiri alichaguliwa kuwa Sheikh wa Tarafa ya Mtae, nafasi aliyoihudumu hadi umauti. Aliheshimiwa na viongozi wa dini, serikali, na jamii kwa ujumla. Pia Alichaguliwa kuwa Mwenyekiti Wa Bodi Ya Shule Ya Secondary Kalumele iliyoko Kijiji Cha Kalumele. 9.TABIA NA MWENENDO WAKE ●Sheikh Muhammad Mzimbiri alijipamba kwa tabia njema zenye kusifika na kutamaniwa, alikuwa mtu mwenye utulivu mkubwa, mwenye hekima na busara katika mazungumzo yake. Alikuwa akipendelea kunyamaza zaidi kuliko kuzungumza ovyo, na kila alipozungumza, aliongea kwa kauli fasaha, zenye maana, na zenye kujenga. ●Uchamungu na ibada: Shekh Alikuwa mcha Mungu wa kweli, asiyeacha swala hata katika mazingira magumu, akikesha kwa ibada, hususan Qiyamul-Layl, na daima alionekana akiwa na tasbihi mkononi akimdhukuru Allah(s.wt). ●Unyenyekevu: Pamoja na elimu yake, hakuonyesha kibri wala kujiona bora kuliko wengine. Alikaa na watu wa kila aina—maskini, matajiri, vijana, wazee—kwa usawa na upendo, akipenda sana watoto wadogo na kucheza nao. ●Uvumilivu: Alivumilia mateso kama njaa na ugumu wa maisha na changamoto nyingi bila kulalamika. aliwavumilia na kuwapa udhuru hata wale waliokuwa wakimchukia, kumuwekea shonde na kuonyesha uadui kwake, Alipenda kusema: “Subira ni ufunguo wa faraja.” ●Upole na huruma: Alikuwa mpole kwa watoto, mwenye huruma kwa wajane na yatima, alikipenda kuwafariji wale waliomjia wakishtakia mazito yanayo wakabili. ●Uadilifu na ukweli: Hakuwa na hila wala udanganyifu. Alijulikana kwa kutotetereka katika kusema kweli hata kama ungekuwa mchungu, alimtanguliza Allah kwa kila jambo hakuibeba Dunia. ●Heshima kwa wazazi na walimu: Alimpenda sana mama yake Bibi Suse, na Baba yake Mzee Mussa Mzimbiri na wazazi wake wengine hadi hapo walipo fariki alikuwa akiwatizama kwa ukaribu. Alikuwa mtiifu kwa walimu wake na hakuwahi kuwazungumzia vibaya hata baada ya kuwa Sheikh. MAJUKWAA ALIYOTUMIA KUENEZA DINI Shekh Muhammad Mussa Mzimbiri Alitumia Majukwaa (Mimbari) mbalimbali katika kuihubiri Dini na Kufikisha Ujumbe wa kiislam, ambapo miongoni mwa majukwaa hayo ni kama Madaarisi(Madrasa) Misikiti Majukwaa Ya Mikusanyiko ya matukio maalum yanayo wakutanisha waislam Kama vile Misiba, Khitma, Maulid ya Mtume Muhammad(s.a.w) Na katika Mikusanyiko Mikubwa Ya Ijtimaai inayo kusanya watu kutoka kila kona ya Tanzania 10.KIFO NA MAZISHI YAKE; TAREKH YA KUFA KWAKE: Shekh Muhammad Mzimbiri alifariki dunia tarehe 19 Desemba 2020, kwa ajali ya pikipiki aliyoipata akiwa na mwanafunzi wake Wifaqa Ally Sharafin aliyekuja kusoma akitokea Mkoa Wa Mtwara, ajali iliyotokea wilaya ya korogwe barabara ya kutoka mombo kuingia korogwe ambao walikuwa wakielekea Tanga Mjini kushiriki katika hauli ya Sheikh Muhammad Ayoub. MAZISHI YAKE; Mazishi yake Shekh Muhammad Mussa Mzimbiri yalifanyika kijijini Tema, nyumbani kwake, ambapo alizikwa tarekh 21 December 2020 nyuma ya madrasa yake aliyojenga. Watu mamia walihudhuria, kutoka mikoa mbalimbali ya Tanzania Mashekh mbalimbali na wanafunzi wake wakilia kwa huzuni lakini wakikumbuka maisha ya mtu aliyewapenda, kuwaongoza na kuwaelimisha, hadi leo kaburi lake linatembelewa na wanafunzi wake pamoja na watu wanaothamini mchango wake katika Jamii. 10.HITIMISHO Sheikh Muhammad Mussa Mzimbiri alikuwa si tu mwanazuoni, bali mlezi wa jamii, kiongozi wa kiroho, na kioo cha elimu na adabu. Alitoa maisha yake yote tangu yungali mdogo katika kuutumikia Uislamu na Waislamu na kuinua kizazi cha wanafunzi waliobeba bendera ya dini ya Kiislamu na maadili mema. Alikuwa nguzo Muhimu ya Dini na Jamii, alikuwa alama ya Ustahmilivu na mfano bora wa malezi ya kiislamu, aliacha pengo kubwa lisiloweza kuzibika kwa urahisi, katika historia ya Mashekh wa Milima ya Usambara jina lake litaendelea kuandikwa kwa wino wa dhahabu na katika nyoyo za wale waliomjua litabaki hai daima. > “Ulimwengu utamkumbuka, historia itamuhifadhi, na malaika watamshuhudia.” Allah amraham Shekh Muhammad Mzimbiri amsamehe madhambi yake ampe daraja za juu peponi, alinawirishe kaburi lake, alifanye kuwa bustani miongoni mwa Bustani za peponi, awazidishie mema wanawe na wanafunzi wake waliochuma nuru ya Elimu kutoka kwake na aturuzuku kufaidika na elimu, barka na athari zake. Aamiin. Imeandikwa na Mtoto wake Alfaqeer Sufian Muhammad Mzimbiri Allah Ampe Fat'hi na Amhifadhi Hali ya kuwa naye ni Mwenye Kunukuu Kutoka katika kinywa Cha Mudiri Wa Tawi La Madrasat Shamsiya Tema Shekh Ja'far Mussa Mzimbiri Allah Amhifadh na Atunufaishe Kwa Barka Na Ilmu Yake aamiin Tar, 30 MAY, 2025

Comments

  1. Maa’shaAllah. Allah amlipe jazaa kwa ilmu yake na amsamehe dhambi zake na amuingize Jannah.

    ReplyDelete

Post a Comment

Popular posts from this blog

WANAUME WENGI WAKIJA KUFANIKIWA HUBADILIKA NA KUNYANYASA WAKE ZAO